BINADAMU amekuwa mshabikiaji wa
mambo kwa lengo la kujipatia mafanikio hata kama njia anazozitumia ni chafu hali
inayopofusha maisha ya utakatifu.
Haya yamezungumzwa Rais wa Baraza
la Maaskofu Tanzania Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa wakati wa
maadhimisho ya Misa Takatifu iliyofanyika katika Kanisa la Moyo Mtakatifu wa
Yesu Parokia ya Tosamaganga katika jimbo la Iringa ikiwa ni maadhimisho ya Siku
Kuu ya Mtakatifu Teresia wa Mtoto Yesu.
Askofu Ngalalekumtwa ambaye pia
ni askofu wa jimbo la Iringa na mlezi wa jimbo Kuu la Songea amesema binadamu
wa leo wamekuwa wagumu kushauriwa na kuonywa kwa kuwa wanatumia njia chafu
kujipatia utajiri.
Amesema kiburi kimetawala na
kusababisha haki za watu kupuuzwa huku wachache wakinufaika kwa kupitia njia
haramu jambo lililo kinyume na mpango wa Mungu.
“Tunashabikia kile tunachoona
kitatuletea raha. Tunashabikia ili kufikia malengo yetu hata kama ni kwa njia
haramu. Tunashabikia majina makubwa, fedha, vyeo hali inayopofusha maisha na
maisha yetu ya utakatifu” amesema Ngalalekumtwa.
Amesema mwisho wa hayo yote ni
machungu na majuto yasiyoisha kwani ni ukaidi wa makusudi kuendekeza kiburi
badala ya upole na unyenyekevu ili kufuata njia sahihi.
Amesema mwanadamu anapoonywa na
kukemewa kwa kile anachokifanya kinyume cha utaratibu na makubaliano ya jamii
au jumuiya ameona kama ananyanyaswa na kuwa na majigambo na kiburi kukaidi onyo
analopata hata ka kama ni kwa faida yake mwenyewe.
“Asituambie mtu kitu, asituonye
au kutukemea, jibu lake ni unyanyasaji na kujenga kiburi kuishi katika
ukengeufu, tumekuwa na majigambo na kiburi, hatutaki kuambiwa kitu na mtu
yeyote na hata sauti ya Mungu tumeizibia masikio” amesema.
Amesema kila mmoja anapaswa
kujiuliza kama anaishi katika haki na uadilifu kwa kushirikiana na wengine
katika katika kuwatendea wengine matendo mema.
Amesema kuishi vizuri hapa
duniani ni kutengeneza histori na kumbukumbu ambayo itaigwa na wengi kama watakatifu
walivyofanya katika maisha yao.
Hata hivyo amesema binadamu
ameteuliwa na Mungu ili aweze kuishi katika haki na uadilifu kwa kuwajali wale
wote wanaohitaji kupata huduma na msaada.
“Tumeteuliwa na Mungu kuishi
katika haki na uadilifu. Sisi walimwengu wa leo tunajiwekea malengo ambayo
tunaamini yatashibisha mahitaji yetu na tumeshindwa kupekua neno la Mungu
lakini mambo mengine tuna muda.
“Uteuzi huo unatutaka kufanya
kile Mungu anataka tufanye na kuishi katika maisha mazuri yenye Baraka katika
kuwatumikia wanadamu wenzetu” amesema.
Amesema maisha ya mwanadamu
yamekuwa ni ya ubabaishaji na kufanya mambo hovyo bila kujali hukumu anayoweza
kupata kutoka kwa Mungu.
Amesema Imani ndiyo inayompa mtu
ujasiri wa wa kutetea haki na wajibu wake kwa kumtumikia Mungu na wanadamu
wenzake katika uadilifu na ustahimilifu.
“Tujenge urafiki na watakatifu
maana wao wana hamu nasi. Watakatifu ni washenga wetu, ni daraja linalotupeleka
uzimani. Swali la kujiuliza ni kwamba, tunaishi katika haki? Tukiishi vizuri
hapa duniani, tutakumbukwa kwa matendo yetu” amesema.
Amewataka wakristo kuwa na tamaa
ya kufika mbinguni waliko watakatifu na malaika wanaotamani binadamu kufika
huko waliko kwa kuishi maisha yanayompendeza Mungu.
“Watakatifu wanatamani sisi
tuishi vizuri, tuishi vema ili tuweze kuufikia utakatifu huko mbinguni” amesema.
Pia amesema binadamu wawe na ujasiri
wa kutetea na kusimamia imani zao na uinjilishaji kwa ajili ya kusaidi roho za
watu ziweze kupata wokovu na kuufikia uzima wa milele.
“Kuweni n a ujasiri wa kutetea
Imani na uinjilishaji ili roho za wanadamu zipate kufunguliwa na kuenenda
katika Kristo” amesema.
Wakatoliki pia wameashwa kuwa na
moyo wa kujitolea kwa ajili ya kujenga familia ya Mungu yenye upendo na amani
kwa kuishi katika mshikamano na umoja.
Amesema magumu yanayotokea isiwe
sababu ya mwanadamu kumuacha Mungu na kukimbilia njia zisizo halali katika
kutafuta suluhu bali Kristo pekee ndiyo jibu la kila jambo na kwamba mwanadamu
anakabiliwa na changamoto kubwa ya kupambana na vishawishi vinavyorudisha Imani
na kukatisha tamaa ya kumtafuta Mungu.
Amesema kila mtu anapaswa kuwa na
hekima, busara, kuwa mpole na mnyenyekevu kwa ili kuwa na mahusiano mazuri na
wenzake kwa ajili ya kulinda na kudumisha amani ya taifa ili jamii iweze kuishi
kwa furaha kila wakati.
“Roho wa Mungu atawale kila
sehemu maana yeye ni roho wa hekima, upendo, upole, ushuhuda na ukarimu. Tuishi
katika hayo ili tuweze kuongezwa thawabu kubwa ya maisha hapa duniani na
kujiongezea hazina ya uzima huko mbinguni” amesema.
Amesema kuishi maisha ya utakatifu kunahitaji moyo wa
kujitoa na kuacha mambo mengine ambayo ni ya anasa na kuacha kupenda kufanya
mambo kwa njia zisizo halali kwa kutaka kupata mafanikio ya haraka.
“Sisi wanakanisa tujawe na moyo wa kujitoa, moyo wa huruma,
ukarimu ili tuwasaidie wahitaji wote. Tuendelee kuishi katika upendo
aliotuachia Kristo kwa ajili ya utukufu wake. Tusiwe na chokochoko za kuvuruga
amani. Tulinde imani yetu katu katika hali ya utulivu na heshima tukimtukuza
Mungu wengu aliye juu” amesema.
Amesema kejeli kwa watu wengine zisifanyike na badala yake
kila mmoja atumie nafasi yake katika kumuomba Mungu.
Amesema wakristo watumie muda wao kutangaza injili
kupenyeza kwenye mioyo ya watu ili hata wale wasiomfahamu Kristo waweze
kumtambua na kumfuata.
“Kwa maombezi ya Mtakatifu Teresia wa Mtoto Yesu, tuwe na
moyo wa ukarimu ili Kanisa lijieneze, lipenye mioyo ya watu. Kwa maombezi ya
Mt. Teresia wa Mtoto Yesu, Mungu awalinde na kuwatunza ili mdumu katika moyo wa shukrani” amesema.
No comments:
Post a Comment