| Maandamo yakiingia katika eneo ambalo Misa Takatifu ilifanyika katika maadhimisho ya uzinduzi wa Yubilei ya Miaka 5o ya Parokia ya Ng'ingula. |
| Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa akiwasha mshumaa wa Yubilei wakati wa maadhimisho ya Misa Takatifu. |
| Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa akiwaonesha waamini mshuma wa Yubilei baada ya kuuwaswha. |
| Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa akihubiri wakati wa maadhimisho ya uzinduzi wa miaka 50 ya Yubilei ya Parokia ya Mtakatifu Petro Claveri Ng'ingula. |
| Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa akitoa Sakramenti ya Kipaimara kwa mmoja wa vijana 368 waliopata Sakramenti hiyo. |
| Eliasa Mdeke aliyeingia na silaha aina ya sime katika eneo la Ibada ya Misa Takatifu na kusababisha usumbufu kwa baadhi ya waamini. |
| Silaha aina ya sime ikiwa chini baada ya walinzi kuinyang'anya mikoni kwa Eliasa Mdeke aliyeingia nayo katika eneo la Ibada ya Misa Takatifu. |
| Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa akipokea keki. |
| Mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa akiwa na Paroko wa Parokia ya Ng'ingula Padre Petro Choga na wawakilishi wa mashirika ya kitawa wakikata keki. |
SIME yaleta kizazaa wakati wa
ibada ya Misa iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Petro Claveri
Parokia ya Ng’ingula jimbo la Iringa baada ya kijana mmoja kuingia nayo katika
eneo la ibada.
Kizazaa hicho kilikuja baada ya
mgambo waliokuwa wakilinda usalama katika maeneo hayo kumtilia shaka kijana
mmoja ambaye aliingia eneo la ibada akiwa mgeni na hali iliyosababisha walinda
usalama wa maeneo hayo kuanza kumfuatilia hadi walipo mkamata.
Wakizungumza na mwandishi wa
habari hizi kanisani hapo mara baada ya kumkamata walinzi hao walisema baada ya
kufanikisha zoezi la kumfuatilia na kumkamata walimpekuwa na kumpata na silaha
aina ya sime.
Akizungumza kwa niaba ya
walinzi wenzake Jadili Kidava MG 424567 alisema kijana huyo aliingia eneo la
ibada akiwa amebeba kibegi aina ya lasketi ambapo kwa namna alivyoingia
walimtilia shaka na uanza kumfuatilia.
“Tulimtilia shaka na kuanza
kumfuatilia lakini kila anapotuona alikuwa anajificha tukajipanga kw ajili ya
kumtafuta ili tuhojiane naye. Mitego yetu ilifanikiwa tukampekuwa tukamkuta na
silaha aina ya sime lakini tulipoaanza kumhoji sababu ya kuwa na silaha hiyo
maeneo ya kuabudu hakutupatia majibu” alisema Kidava.
MG 395524 alisema ilikuwa kazi
kumtafuta kwenye kundi la watu ili watu wasipate wasiwasi japo ilichukua muda
kumkamata kutokana na wingi wa watu waliokuwepo kwenye ibada.
Hata hivyo baadhi ya watu
walioiona sime hiyo walianza kukosa amani hali iliyosababisha watu waliokuwepo
getini kukimbia.
Akihojiana na mwandishi wa
habari hizi kijana huyo alijitambulisha kwa jina la Eliasa Mdeke ambapo alisema
anatoka katika kijiji cha Mbawi ambapo alisema silaha ni kwa ajili ya usalama
wake.
Alipotakiwa kueleza ni
kiashilia gani kimemfanya atembee na silaha kwa ajili ya usalama wake, hakuwa
na majibu.
Hata hivyo alisema hana makazi
maalumu licha ya kusema wazazi wake ni Victor Mdeke na Esta Katindasa hata
alipotakiwa kuwataja viongozi wake wa kijiji alisema hawafahamu.
Kila alipotakiwa kutoa
ufafanuzi zaidi kutembea na silaha hiyo Mdeke alisisitiza kuwa ni kwa ajili ya
kujihami kiusalama zaidi.
Ofisa mtendaji wa kijiji cha
Ng’ingula Bakari Kpopele alisema anamuweka chini ya ulinzi hadi atakapotoa
maelezo ya kutosha.
“Natakiwa kupata majibu kwa
nini ameingia na silaha kanisani ndipo uamuzi ufanyike. Hapa ni sehemu ya
kuabudu na watu wengi wamekusanyika hapa sasa unapoingia na silaha unamaanisha
nini! Majibu nitayapata” alisema.
Akihubiri katika Misa hiyo Rais wa Baraza la maaskofu
Tanzania mhashamu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa alisema wakristo wasigeuke
kuwa waagizaji ndani ya Kanisa kwa kufanya mambo machafu na kuwakosesha amani wengini.
Alisema Kanisa ni chombo cha kuwabeba wanadamu kuwapeleka
uzimani na kwamba binadamu hawezi kuwa mfuasi wa Kristo iwapo anakuwa na
matatizo duniani.
Alitaja mambo yanayoweza kumkosesha mtu kuwa wafuasi wa
kristo kuwa ni hali ya dunia kuwa na mambo ya anasa yasiyo na maadili, kutotoa
huduma ya kweli na haki kwa wanadamu wengine, iwapo binadamu hatakuwa msaada
kwa wengine, kutokuwa na mawasiliano yaliyo mazuri na kusababisha mvurugano kwa
wengine na kutokuwa na vitendea kazi vizuri na kusababisha malalamiko kwa
wengine.
Alisema mwanadamu amekuwa mtumwa wa dunia kwa kufanya mali
za dunia kuwa miungu wake na kutumia nafasi yake kuwaumiza wengine.
“Mali za dunia hii zisiwe kikwazo cha kumtafuta Mungu; mali
ya dunia hii tuitumie lakini isiwe chanzo cha utumwa kwetu bali tuwe na uhuru
wa kuleta amani” alisema.
Askofu Ngalalekumtwa ambaye pia ni askofu wa jimbo la Iringa
na msimamizi wa jimbo la Songea, alisema daima binadamu anasisitizwa kuwa
mnyenyekevu kwa Mungu na kwa wenzake akiwa mpole, huruma na amani.
“Tusijiite wakristo wakati si kitu mbele za wenzetu kila
siku tunasababisha migogoro na kusababisha kubomoa familia ya Mungu. Je, roho
yangu ni ya huruma? Kila mmoja awajibike katika nafasi yake bila kuwa kikwazo
kwa wenzake” alisema.
Alisema utulivu wa kila mmoja ni ulinzi wa amani kwa kila
mtu na kuifanya familia ya Mungu ambayo ni wanadamu aliowaumba kuishi kwa
upendo na furaha.
Akizindua yubilei ya Miaka 50 ya Parokia hiyo, askofu
Ngalalekumtwa alisema mwaka wa Yubilei uwe ni mwaka wa kujitafakari,
kujitathimini, kujipekua, kujichunguza, kujitafiti na kujisahihisha .
Alisema kila wakati binadamu amekengeuka na kufanya
yasiyompendeza Mungu na kuwa na mapungufu mbele ya Mungu nay a wenzake huku
akiwa mgumu kubadilika na kusababisha mwenendo wake kuwa mbaya.
“Kila mmoja akae na kutulia nafsini mwake kwa kulinda amani,
kujenga utamadumi wa toba, upendo na kuzingatia utulivu” alisema askofu
Ngalalekumtwa.
Alisema kukosa imani na amani ni sawa na mtu anayetembea
akiwa na vidudu vya ajabu ajabu mwilini mwake na kwamba maisha ya mwanadamu
hapa duniani ni ya kupita tu ambapo anatakiwa kuishi katika hali ya usafi kila
wakati.
“Mwaka huu wa Yubilei uwe ni mwaka wa kumtangaza Kristo na
kuchochea amani kwa watu wote duniani. Daima tumwombe roho wa hekima atutie
moyo wa hekima ili tuishi katika utangazaji wa injili ya Bwana kwa kuishi kwa
amani pasipo fujo , mvurugano na kuishi kwa kuheshimiana.
“Kila mmoja awe wakala wa heshima, amani, furaha na upendo
kwa wengine; tusiwafanye wengine kuwa watumwa wetu kwa yale tunayoyafanya kwa
kutaka kuabudiwa” alisema.
Aliwataka wazazi na walezi kuwalea watoto wao katika misingi
ya haki na msamaha ili waweze kukua wakiishi katika kuheshimiana, upendo na
ushirikiano bila kubaguana.
Pia amewataka wale wanaoshikilia nafasi katika njanja
mbalimbali za kuwaongoza wenzao wasitumie nafasi zao kuwanyanyasa na
kuwanyang’anya haki zao na badala yake kupitia nafasi hizo, watu waonje uwepo
wao kwani uwajibikaji mzuri ni kuwa na hofu ya Mungu.
Akisoma risala mbele ya Mhashamu askofu Ngalalekumtwa Sixtus
Mtenga ambaye pia ni katekista wa kigango cha Ng’ingula alisema mwaka wa
Yubilei umepokelewa vizuri ambapo wanatarajia kuwanya mambo mbalimbali ya
kiroho katika kukuza imani.
“Tumeanza kushiri semina mbalimbali. Katika mwaka huu
tutajitahidi kuwa na vipindi mbalimbali vya kiroho ili tuweze kukuza imani
ikiwa ni pamoja na kusaidiana kuwafikia wale wenye hamu na kiu ya Mungu ili
waweze kupata huduma wanazostahili’ alisema.
Parokia ya Mtakatifu Petro Claveri ilianzishwa mwaka 1964
Itanga ambapo mwaka 1973 ilihamia rasmi Ng’ingula chini ya uongozi wa shirika
la wamisionari wa Bikira Maria Consolata ambapo hadi sasa parokia ina jumla ya
wakristo wabatizwa 13,250.
Maadhimisho ya uzinduzi wa Yubilei hiyo yalikwenda sambamba
na utoaji wa Sakramenti ya Kipaimara na jumla ya vijana 368 walipewa Sakramenti hiyo
ambapo kilele cha Yubilei hiyo kinatarajiwa kufanyika mwakani (2014).
No comments:
Post a Comment