![]() |
| Balozi wa China nchini, Dk. Youging (kulia) akiwa kwenye mkutano wa CCM. Kulia ni Nape Nnauye na Abdulrahman Kinana. (katikati) |
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wapeleka mashtaka rasmi kumshtaki Balozi wa China kwa umoja wa mataifa (UN).
Balozi wa china hapa nchini Dkt. Lu Youging ameshtakiwa rasmi hii leo na Chadema kwa umoja wa matifa kwa kile kilichoelezwa kuwa anafanya uenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kinyume cha makubaliano ya sheria za umoja wa mataifa ya mwaka 1961 kuwa ni kosa kwa Balosi yeyote kufanya siasa katika nchi isiyo ya kwake.
Mashtaka hayo yamekuja siku moja baada ya Mkurugenzi wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Chadema, Ezekia Wenje, alipozungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam kuwa Balozi huyo amevunja
mkataba unaowaongoza mabalozi ujulikanao kama ‘Vienna Conversion on Diplomatic
Relations’.
Wenje ambaye pia ni Mbunge wa Nyamagana, mkoani Mwanza, alisema
mkataba huo unazungumzia mahusiano ya kibalozi baina ya nchi na nchi na kazi za
balozi awapo kwenye nchi fulani kwamba siyo kujihusisha na mambo ya ndani ya
nchi husika zaidi ya kujenga mahusiano baina ya nchi hizo na kusaidia wananchi
wa nchi yake na wananchi husika wanaotaka kwenda kwenye nchi yake.
“Ibara ya 41 (1) inakataza mabalozi kujiingiza katika masuala ya
ndani ya nchi ikiwamo siasa, ibara ya tatu ikionyesha kazi za balozi na ibara
ya 31 (1) inazungumzia kinga ya balozi, kama atajiingiza kwenye kazi ambazo
hazimuhusu kinga itaondolewa,” alifafanua Wenje.
Alisema kazi ya balozi ni kutengeneza uhusiano baina ya
nchi yake na Tanzania na siyo kuwa mwenezi wa chama chochote cha siasa na
kwamba alichofanya balozi huyo ni kugeuka kuwa Katibu Mwenezi wa CCM huku
akisakata muziki wa chama hicho hadharani.
Alisema kimsingi, balozi huyo hakutakiwa kushiriki kwenye
mkutano huo na mikutano anayopaswa kushiriki ni ya kiserikali, lakini alisimama
kuhutubia wananchi akiwa amevaa sare ya CCM.
“Tusingependa uhusiano wa kihistoria kati ya China na Tanzania
ambao umedumu kwa muda mrefu tangu uhuru uingizwe matatani au shakani kwa
sababu ya mapenzi binafsi ya balozi kwa CCM,” alisisitiza Wenje.
Balozi huyo
alikaririwa na vyambo vya habari wakati akihutubia mkutano wa hadhara akiwa na
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, na kujitahidi kuwasalimia wananchi hao
kwa lugha ya kabila la Wasukuma kwa kusema mwadila.
Alisema pamoja na Tanzania kuwa na mfumo wa vyama vingi,
anaamini kuwa CCM bado iko imara na inaweza kuendelea kuongoza kwa muda mrefu.
“Kwa hili inadhihirisha kuwa hakuna chama kama CCM kutokana na
uimara wake na hili wanalofanya sasa la kuja kuimarisha chama nasi kule China
kupitia chama chetu tawala cha CPC (Chama Cha Kikomunisti cha China), tunafanya
kama hivi pia. Mwadila, Shinyanga, CCM Oyeeeeee asanteni sana,” alikaririwa
akisema.
Wakati huo serikali kupitia
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, imesema kuwa
kitendo kilichofanywa na Balozi huyo siyo sahihi na kinakiuka mkataba wa
Vienna.
“Wizara inapenda kutamka kwamba kitendo cha Balozi yoyote
kuhudhuria mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na kuvaa sare zenye nembo ya
vyama vya siasa siyo sahihi na kinakiuka Kifungu cha 41(1) cha Mkataba wa
Vienna wa mwaka 1961, unaoongoza uhusiano wa kidiplomasia,” alisema Membe
katika taarifa yake jana jioni.
Taarifa hiyo ilisema kuwa mkataba huo unazuia wawakilishi wa
nchi za nje kujihusisha na ushabiki wa kisiasa wanapofanya kazi zao kwenye nchi
za uwakilishi.
“Katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2012, Wizara ilikumbana na
vitendo vinavyofanana na kitendo hiki na ikachukua hatua stahiki, kadhalika kwa
tukio hili Wizara itachukua hatua za kidiplomasia zinazostahili ili kuzuia
jambo hili lisitokee tena,” alisisitiza.
Alisema Wizara imeona
picha na habari kwenye vyombo vya habari zikieleza na kumuonyesha Balozi huyo
akiwa kwenye mkutano wa CCM
Balozi huyo alikwenda wilayani humo kuhudhuria uzinduzi wa mradi wa viwanda vya kuchambua pamba vinavyojengwa na mwekezaji wa Kichina anayeitwa Tahong ambapo viwanda hivyo vinatarajiwa kuwa na uwezo wa kuchambua tani 120,000 za pamba kwa mwaka vitakapokamilika mwakani.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alipotafutwa kutoa ufafanuzi juu ya suala hilo, hakupatikana kutokana na simu zake za kiganjani
kufungwa.
Hata hivyo, Nape juzi alisema atatoa ufafanuzi wa masuala yote
kuhusu chama chake atakaporejea kutoka katika ziara hiyo anayofuatana na
Kinana.

No comments:
Post a Comment