| Jengo la vyoo vya soko jipya linaloendelea kujengwa katika mtaa wa Ngome Kata ya Kihesa Manispaa ya Iringa linalodaiwa kujengwa kwa gharama ya shilingi 15 milioni. |
WAKAZI wa Mtaa wa Ngome Kata ya
Kihesa katika Manispaa ya Iringa, wamemtaka Mkurugenzi wa Manispaa kuunda tume
ya wataalamu wa majengo ili kuchunguza uhalali wa ujenzi wa jengo la vyoo
katika soko jipya linaloendelea kujengwa katika Mtaa huo.
Wakazi hao wameeleza kuwa
wamefikia uamuzi huo kutokana na kutokuridhika na taarifa za gharama ya ujenzi
wa jengo hilo
na ukubwa wa jengo lenyewe.
Kwa nyakati tofauti wamesema
kumekuwa na ubabaishaji wa ujenzi huo hali iliyosababisha hata mwenyekiti wa
mtaa kutafutiwa makosa kwa kuwa amekuwa akisema ukweli.
Wameeleza kuwa lango la kutaka
ufanyike uchunguzi ni kutaka kujua idadi ya bati zilizotumika, mifuko ya
sementi mingapi, mawe kiasi gani, nondo kiasi gani na za aina gani, tripu ngapi
za mchanga na tofati, misumari kiasi gani pamoja na mbao ngapi
“Siwezi kukubali hata kwa moto
kuamini gharama za ujenzi huo. Kama gharama
hizo ni za kweli, kwa nini ofisa mtendaji wakati anatoa taarifa alisoma barua
ya kumsimamisha uenyekiti mwenyekiti wetu wa mtaa?” amesema mkazi mmoja.
Wamesema kila wakati wamekuwa na
wasiwasi na taarifa alizokuwa akizitoa ofisa mtendaji wa mtaa huo kwa kile
walichoeleza kuwa taarifa hizo zina utata muda wote.
“Huyu mtendaji wa mtaa huu
hatumuelewi. Na ukifuatilia kwa umakini anashirikiana na watu wakubwa tu ili
kupitia ujenzi wa soko hili kwa manufaa ya familia zao. Asifkiri kuwa watu
wajinga. Tujua kila kinachoendelea lakini umefika muda wa kumwambia hatuna
imani naye” amesema mkazi mwingine.
Mkazi mmoja anayeishi jirani na
soko hilo ambaye ameomba jina lake lisiandikwe
gazetini ameeleza kuwa mara kadhaa amewaona watu wakipita na sementi usiku na
kuingiza kwenye nyumba moja ambaye jina tunalo.
“Mimi nimekuwa nikishuhudia
semementi ikichukuliwa usiku kuanzia saa tano watu wakiwa wamelala. Utakuta
watu wanachukua sementi na kuingiza kwenye nyumba moja hapa jirani. Wanafikiri
wakituambia tu taarifa za ujenzi sisi ni wajinga tutakubali tu. Hizo ni kodi
zetu tunazokamuliwa kila siku huku tukishindwa hata kununua chakula chetu tu.
Bora ufanyike uchunguzi wa umakini tujue ukweli. Nakuhakikishia, ukifanyika
uchunguzi wa uhakika haponi mtu hapa” kimesema chanzo chetu.
Machi 16, 2013 ofisa mtendaji wa
mtaa huo Eliques Ngakonda akisoma taarifa ya ujenzi katika mkutano wa hadhara
uliofanyika katika viwanja vya soko hilo na
kuhudhuliwa na watu 32 alisema kuwa ujenzi wa jengo hilo la vyoo umegharimu 15 milioni bila
kuainisha matumizi hayo jambo lililowafanya watu kuwa na miguno ya kila aina.
Sambamba na taarifa ya ujenzi
ofisa huyo alisema hamtambui mwenyekiti wa mtaa huo Elizabeth
Mkayula kama mwenyekiti kwa kuwa
ameshaondolewa katika kiti hicho na kumkaimisha Prisca Mkusa hali
iliyosababisha watu waliohudhuria katika mkutano huo kupinga vikali.
“Huyo tulimchagua sisi na
tutamtoa sisi. Hatujamfukuza, huyo mnayemuweka wa kwenu. Mnamtoa mwenyekiti
wetu kwani ninyi ni akina nani” zilisikika sauti hizo.
Hata hivyo utafiti uliofanyika
umebaini kuwa kuenguliwa kwa mwenyekiti huyo ni ujenzi wa soko hilo kwa kuwa
baadhi ya watu wanashindwa kuiba kwa kuwa mwenyekiti ni muazi na ni mkweli.
“Yapo mengi juu ya ofisa mtendaji
huyo na wenzake anaoshirikiana nao lakini kilichokikubwa ufanyike uchunguzi wa
ujenzi wa soko hilo
kwanza” kimesema chanzo chetu.
Licha ya milioni 15
zinazosadikiwa kujenga vyoo hivyo, imeelezwa kuwa mashimo pekee yalijengwa kwa
shilingi milioni 8 tofauti na zile 15 milioni zinazozungumziwa.
Mtu mmoja miongoni mwa wale wa
kamati ya ujenzi ambaye ameomba jina lake
lisiandikwe ameeleza kuwa
kuna ujanja mkubwa umefanyika ambao ni wa machomacho.
“Zimekuwa zikitumika mbinu za
ujanja. Kwa upande wangu siwezi kukubali na siwezi kusaini kuwa 15 milioni
zimejenga jengo lile kwa sababu najua mbinu zilizotumika” amesema.
Mwenyekiti wa mtaa huo Elizabeth
Mkayula alipotafutwa kutoa ufafanuzi zaidi alisema hawezi kusema chochote kwa
kuwa hakushirikishwa.
“Siwezi kusema lolote kwa sababu
ujenzi huo sikushirkishwa ila tu nilikuwa nikipigwa vita ili nisifuatilie
kinachofanyika pamoja na kuwa mwenyekitu wa mtaa ndiye anayetakiwa kuwa mfuatiliaji
wa karibu katika masuala kama hayo kwa sababu ndiye anayewajua watu wake na
kuongea na watu wake juu ya maendeleo. Kwa kweli nisiwe muongo hapo sijui
lolote” amesema Mkayula.
No comments:
Post a Comment