| Mkuu wa Wilaya ya Kilolo Gerald Guninita |
MRADI wa umeme wa upepo uliotarajiwa katika Wilaya ya Kilolo umeota mabawa kutokana na miundombinu.
Mkuu wa Wilaya ya Kilolo Gerald Guninita ameliambia mtandao huu ofisini kwake kuwa mradi wa umeme wa upepo uliotarajiwa kuanza mwaka huu umekwama kuokana na wataalamu kudai kuwa miundombinu haitafanikisha kusafirisha mitambo.
Guninita ameutaja mlima wa Kitonga ndio ulioelezwa kuwa ni kikwazo kwa usafirishaji wa mitambo hiyo kutokana na ukali wa kona na urefu wa nguzo hizo.
“Mwaka huu mradi ulikuwa uanze rasmi katika Wilaya yetu lakini kwa bahati mbaya wataalamu wamesema haitawezekana kutokana na mlima wa Kitonga kuwa na kona kali na nguzo kuwa ndefu” alisema.
Alisema kutokana na tatizo hilo, mradi umehamishwa kwenda Mkoa wa Singida ambako kumeonekana kuwa na upepo mwingi kama ilivyo katika vijiji vilivyokuwa vinatarajiwa kunufaika na mradi huo katika Wilaya ya Kilolo.
“Hatuna jinsi kwani kama tatizo ni usafirishaji hasa wa nguzo katika mlima Kitonga, si jambo la haraka kwamba tunaweza kutengeneza barabara mbadala ya haraka haraka. Hivyo, mradi unahamia Singida ambako pia kuna sehemu zenye sifa kama huku” alisema Guninita.
Wakati Athumani Mfutakamba alipokuwa Mkuu wa Wilaya hiyo, alisema jumla ya vijiji 10 vitanufaika na mradi huo wa umeme wa upepo.
No comments:
Post a Comment