WAFANYAKAZI wa Kampuni inayojihusisha na ujenzi wa barabara ya
mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) ya Strabag, jana wamegoma
kufanya kazi kutokana na kubaguliwa katika malipo ya stahili na posho.
Akizungumza na mtandao huu jijini Dar es Salaam jana
kwa niaba ya wafanyakazi wenzake, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi
Strabag, Abdullah Rukusa, alisema sababu kubwa ya mgomo huo ni
ubaguzi unofanywa na uongozi wa juu katika suala la malipo ya stahili
zao ya sh 65,000 za wafanyakazi hao.
Rukusa alisema wafanyakazi wa kampuni hiyo hasa wazawa wamekuwa
wakibaguliwa katika malipo na kwamba raia wa kigeni wamekuwa wakipewa
kipaumbele.
Alisema ingawa kesi ya madai yao ipo mahakamani, lakini wanashangazwa
na utaratibu uliopo ambao unawafanya kufanya kazi katika mazingira
magumu, jambo ambalo linazorotesha na kuchelewesha umalizikaji wa
Barabara ya Morogoro.
“Tunabaguliwa sana, haiwezekani raia wa kigeni walipwe posho na
stahili zao sisi Waafrika tusilipwe.
Tunataka haki itendeke katika suala
zima la malipo, vinginevyo wote tusitishiwe malipo,” alisisitiza.
Meneja Uajiri wa Strabag, Nelson Mlumba, alisema hawezi kuzungumza
lolote kwa kuwa wanaingia kwenye kikao ambacho kitakuja na majibu na
suluhisho la matatizo ya wafanyakazi wao.
Chanzo: Tanzania Daima.

No comments:
Post a Comment