![]() |
| Hifadhi ya Udzungwa |
WANANCHI
wa Kilolo wamemtaka Mbunge wao Prof. Peter Msolla (CCM) kutorudi tena kuomba
kura kwao kama hatatekeleza ahadi zake
alizowaahidi mwaka 2011 wakati wa kampeni za uchaguzi Mkuu.
Wananchi
hao wamesema wamefikia hatua hiyo kutokana na Mbunge huyo kuwahadaa kwa mambo
mengi ambayo hajawahi kutekeleza hata moja huku akipotea jimboni kwa muda mrefu
baada ya kupata alichokuwa akihitaji.
Wakizungumza
na mtandao huu, wakazi wa kijiji cha Udekwa Kata ya Udekwa Wilaya ya Kilolo
mkoani Iringa wamesema hawakutarajia kama
kiongozi mwenye hadhi ya uprofesa angeweza kuwadanganya watu.
Wamesema
kwa kutumia cheo chake aliahidi mambo mengi ikiwemo barabara, minara ya simu na
mambo mengine mengi ambayo hadi sasa hakuna hata moja lililoonekana kufanyika
zaidi ya wananchi kunyanyasika.
Katika
hatua nyingine wananchi hao wakiongea katika mkutano wa hadhara wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) uliofanyika kijijini hapo juzi, wamesema
ikiwa wao ndio wapo jirani na hifadhi ya Udzungwa hawaoni manufaa ya hifadhi
hiyo kutokana na kuwa na viongozi wazushi, waongo na vipofu ambao hawaoni
umuhimu wa hifadhi hiyo.
“Tulitegemea
Mbunge alipoahidi barabara hii kujengwa tutanufaika na hifadhi hii kwa sababu
ya kufikiwa kwa urahi na watalii lakini cha kushangaza imekuwa ni rahisi
kusafirisha mzigo kutoka mjini kwenda Dar es Salaam kwa bei nafuu kuliko kutoka
hapa kijijini kwenda Mjini.
“Utashangaa
gunia moja la maharage linasafirishwa kwa shilingi elfu nane hadi elfu kumi
kutoka hapa kijijini kwenda Iringa mjini wakati gunia hilo
hilo linasafirishwa kwa shilingi elfu tatu
kutoka Iringa mjini kwenda Dar es
Salaam . Hii inatokana na viongozi wetu kuwa wanafiki
na waongo kutufanya sisi watoto” alisema Baraka Mfilinge.
Wananchi
wao wamesema itafika mahali ambapo watafanya maandamano hadi halmashauri ya
Kilolo kudai barabara kwa kuwa ni haki yao
ya msingi ambayo wanahitaji kupata kwa kuwa kodi zao zinatakiwa kuwanufaisha.
Akiongea
na wananchi wa Udekwa kwenye mkutano huo, mlezi wa Chadema Wilaya ya Kilolo Brian
Kikoti alisema daktari aliyeshindwa kutambua ugonjwa, hawezi kuutibu na kwamba
viongozi walioshindwa kutambua matatizo ya wananchi hawawezi kuyatatua.
Amesema
licha ya nchi kuwa na sheria, hazifanyi kazi kwa usawa na badala yake
zinapendelea upande mmoja kwa maana ya kuegemea katika Chama cha Mapinduzi
badala ya kusimamia haki za wananchi.
“Ikiwa
diwani anashindwa kuwasemea watu wake, ni sawa na pipa la taka. Ni lazima
tutafakari juu ya watoto wetu na akina mama kuwa ni maisha gani tunataka kuishi
kwa sasa na kwa baadaye. Sisi wenyewe ndiyo tunaojiingiza mkenge kwa kuchagua
viongozi walafi, wanafiki, wababaishaji na waroho.
“Utalii
katika hifadhi zetu utachelewa kwa sababu viongozi tulio nao hawana upeo wa
maendeleo bali wana upeo wa matumbo yao .
Kama wangekuwa na akili ya maendeleo
wangeboresha miundombinu katika ili hifadhi zetu ziweze kufikika kirahisi”
alisema.
Endapo
barabara ya Ilula – Udekwa ingejengwa, ingerahisisha kufikiwa kirahisi hifadhi
ya Udzungwa kwa upande wa Udekwa ambapo hata hivyo Mbunge huyo aliahidi kujenga
barabara ya Mahenge – Mabondwa (Udekwa) lakini hadi leo haijaguswa.



No comments:
Post a Comment