masuguru

Tangazo la cheti

Tangazo la cheti
tangazo

KLERUU

KLERUU
KLERUU

CAPRICORN

CAPRICORN

Ibada

Ibada

Wednesday, October 30, 2013

MKUMBUKENI MUNGU KATIKA SHUGHULI ZOTE: ASKOFU









RAIS wa Baraza la Maaskofu Tanzania Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amewata wakristo kumkumbuka Mungu katika shughuli zao licha ya kuwa wanazongwa na mambo mengi katika pilika za kutafuta mahitaji.

Ameyasema hayo  juma hili wakati wa maadhimisho ya Misa ya mazishi ya hayati askofu mstaafu wa Jimbo la Njombe mhashamu Raymond Mwanyika na kwamba mwanadamu ana kiu ya Mungu.

Bila Mungu binadamu hawezi kupata raha kwa kuwa Mungu ndiye anayemfanya binadamu kuwa na furaha wakati wote na kumuwezesha kufanya kila analolitaka.

Anaendelea kusema ili kuwa binadamu aliyekamilika, lazima kuwa na imani na amani katika kutoa huduma za haki na uwajibikaji wa amani.

Pia anasema ukamilifu wa mtu ni kutumia muda wake kwa ajili ya kupigania usawa na kutaka kila mmoja aweze kupata chochote pasipo kikwazo na kwamba ukamilifu huo unasaidia kuwa na amani moyoni mwake.

Amesema uzuri wa mwanadamu ni pale anapoishi katika haki na amani kwa upendo na kuthamini wenzake kama viumbe wa Mungu bila kuonesha ubaguzi na upendeleo katika utoaji huduma.

Mhashamu askofu Ngalalekumtwa ambaye pia ni askofu wa Jimbo la Iringa na msimamizi wa Kitume wa Jimbo Kuu la Songea anasema moyo wa mwanadamu umejaa mambo mengi ya hapa duniani yenye udanganyifu mwingi ambayo ni kwazo kwa haki za wengine.

“Hupati raha ya kweli pasipokuwepo Mungu. Pamoja na kufukuzia mambo mengi hapa duniani yenye udhaifu mwingi, Mungu anamvuta mwanadamu kwa ajili ya uzima lakini msingi wa hayo yote kinachotakiwa ni kuwa na imani na upendo kwa kila mmoja.

“Ni vema mwanadamu akayaelewa hayo na kutenda kwa maongozo ya Mungu katika hekima na akili. Utamu na unono wa mwanadamu ni pale unapotoa uhai kwa ajili ya wengine katika kutenda haki” ameeleza.


Amesema mtu hawezi kuhubiri amani wakati rohoni mwake hana imani na kwamba kwa kufanya hivyo ni kukosa ukweli ndani ya nafsi yake na kwamba Dini ya ukristo siyo nadharia bali ni msingi wa mafundisho wa yule aliyejitoa msalabani.

“Ukristo ni dini ya ukarimu wa nafsi. Kristo ndiye kitovu na kiini cha kazi ya Mungu. Binadamu wote tumetolewa na Mungu kama zawadi. Mungu anatulinda kwa upendo na kutuhifadhi katika upole na faraja” anasema.

Vile vile anaeleza kuwa binadamu akiwa ni mali ya Kristo lazima ajiule mambo yote anayotenda kwani nia yake ni kutaka wanadamu kujiweka chini ya uhai wa Baba yake.

Akimuelezea hayati askofu Mwanyika, Mhasamu askofu Ngalalekumtwa anasema Alitamani kumsaidia kila mtu lakini uwezo wake haukuruhusu kumfikia kila mmoja na kwamba alikuwa ni mtu mwenye maneno machache na kuongea zaidi kwa matendo

Anasema kuwa hakuwa ni mtu wa kugombana na yeyote, alihudumia kwa ukarimu na kuambatana na wakristo kwa kusudi la wokovu.

“Kanisa Katoliki limejawa na simanzi kuondokewa na askofu wa kwanza wa Jimbo la Njombe. Katika kipindi chote cha uongozi wake, askofu Mwanyika amekuwa kielelezo na kuyatoa maisha yake kwa Mungu na alikuwa mchapa kazi.

“Alifanya bidii kujenga jimbo ili liweze kujitegemea. Alitamani kumsaidia kila mtu lakini uwezo wake haukuruhusu kumfikia kila mmoja. Katika kipindi chake cha uuongozi alihamasisha sana miito. Alikuwa kielelezi katika kuongoza malezi ya watawa jimboni” amesema.

Ameeleza kuwa Maaskofu watamkumbuka jinsi alivyolihudumia Baraza la Maskofu Tanzania na kwamba alikuwa ni mtu mwenye maneno machache na kuongea zaidi kwa matendo.

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa jimbo la Njombe Kusini Mama Anne Makinda alisema hayati askofu Mwanyika alikuwa ni mtu muhimu kwa kuwa alikuwa na dhana ya ushirikiano katika kuleta maendeleo licha ya kuwa alikuwa mtumishi wa Mungu.

“Kanisa limempoteza mtu muhimu sana. Alikuwa na moyo wa maendeleo kwa kuhakikisha watu wake wanakuwa na amani, furaha, upendo na alikuwa ni mtu wa huruma kwa kila mmoja bila kubagua” amesema.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilali alisema Taifa linatambua mchango wa hayati askofu Mwanyika wakati wa uhai wake kwa kutoa huduma kwa upendo na amani.

Anasema kuwa wakati wa uhai wake alikuwa na uelewano kwa kila mtu bila kujali umri wa mtu, cheo na wasifu wake na kutoa huduma kwa haki na kuhakikisha jamii inanufaika kiroho na kimwili.

Amesema kuwa askofu Mwanyika wakati wa uhai wake alikuwa Alikuwa ni mtu mwenye uelewano na ni mtu aliyejenga heshma katika Kanisa la Taifa kwa ujumla.

“Kuweni na ustahimilivu na subira katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo na Mungu awatie nguvu” anasema.

Amewataka watu wote kufuata mafundisho yake ya amani, upendo, umoja na mshikamano kwa kushirikiana kwa kila jambo.

Hayati askofu mstaafu Mwanyika ambaye aliongoza Jimbo la Njombe kwa miaka 31 anaelezwa kuwa atakumbukwa kwa mengi ikiwa ni pamoja na kufanya kazi zake kwa utulivu.

Kwa upande wake Makamu wa askofu wa Njombe Padre Justin Sapula amesema Jimbo la Njombe limempoteza kiongozi makini mwenye busara, mtu wa watu aliyempenda kila mmoja.

Mama Mkuu wa Shirika la Kitawa la Masista wa Imilliwaha Sista Cotride Sanyika akizungumza na KIONGOZI amemwelezea askofu Mwanyika kuwa wakati wa uhai wake alikuwa askofu ambaye hakupenda makuu na kwamba alikuwa ni mtu wa watu.

Anasema alitumia hekima na burasa kuwaongoza watu na kwamba alikuwa ni mtu mpole ambaye daima alikuwa akimtegemea Mungu kwa kila jambo alilokuwa akilitenda.

“Aliwalea Mapadre na Watawa kwa moyo mkunjufu. Hakupenda wakose kitu. Pia alikuwa mbunifu wa hali ya juu na kutumia unyenyekevu katika utume wake. Aliwapenda hata viongozi wa kiserikali kwa kutoa ushirikiano wa dhati kwa kuwa na mawasiliano ya karibu kwa kushiriki shughuli za kimaendeleo” amesema.

Anna Silinu anasema kwa ujumla ni pigo kubwa kwa wananjombe wote kwa kuwa askofu Mwanyika wakati wa uhai wake alikuwa ni mtu wa mfano kwa kila kitu na kuhubiri amani, upendo na mshikano bila ubaguzi.

Anasema wengi wanajifunza kutoka kwake yale aliyokuwa akiyafanya na kuyatenda kwa kutoa ushirikiano katika mambo yote ya kiroho nay a kijamii bila kurudi nyuma.

“Alikuwa ni mtu wa kujitoa bila kujibakiza. Pamoja na kuwa alitoka katika familia masikini alikuwa ni mtu muelewa kwa matatizo ya wanajamii. Alisistiza san asana watu tuishi kwa upendo na amani” anasema.

Amesema katika hali isiyo kuwa ya kawaida hayati askofu Mwanyika wakati wa kuugua kwake alionekana mwenye furaha kushiriki mateso ya Kristo bila manung’uniko.

Silinu amewataka wakristo kutowazuia watoto wao kufuata miito yao kwa kuwa Mungu humuita mtu kwa njia tofauti na kwamba upadre na utawa na wito ambao una baraka na heri katika maisha ya kiroho na kwamba malezi ya kiroho yanategemea uwepo wa watu waliojitoa kiimani.

“Ushirikiano hauwezi kuzaa matunda bila kuwa muwazi na mkweli. Tusiwanyime watoto wetu haki zao” amesema.

Wakati huo huo msemaji wa familia Weliner Mwanyika amesema familia imepata pigo kwa hayati askofu Mwanyika alikuwa nguzo ya familia

Amesema pengo lililopo haliwezi kuzibika kutokana na nafasi yake aliyokuwa nayo na ukaribu wake kwa watu wote katika familia na kutoa mahitaji bila upendeleo.

“Alikuwa akisikia tatizo tu, mara moja alikuwa anawajibika. Alikuwa ni mtu wa karibu na familia. Katika familia tumempoteza mtu muhimu sana” amesema.

Hata hivyo amesema maisha yake yamekuwa mwanga wa imani kwa familia na kuwataka wanafamilia kuyaishi yale aliyokuwa aliyasisitiza kwa kuishi kwa upendo na kuruhusu miito ndani ya familia ili kupata viongozi wa kiroho.

Amesema wajitoe katika yaliyo mema kwa kumtumikia Mungu kwa kufanya ushirikiano na viongozi wa kiroho kuiombea miito mitakatifu na kuwa mwanga wa njia ya haki na kweli katika maisha kikristo.

Pia amesema kujituma ni jambo la heri kwa ajili ya maendeleo ya Kanisa na ustawi wa kiroho kwa kushiriki katika utume mbalimbali na kujitoa kwa uhakika kama hayati askofu Mwanyika alivyokuwa akifundisha na kutenda katika katika maisha yake.

Katika familia hiyo tayari kuna mapadre wawili, Pd. Prasdos Mwanyika na Pd. Osmund Mwanyika.

Askofu mstaafu Raymond Mwanyika wa Jimbo Katoliki la Njombe, alifariki dunia 24 Oktoba 2013, akiwa na umri wa miaka 83. Alizaliwa kunako mwaka 1930. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, akapadrishwa 11 Oktoba 1959. 

Baba Mtakatifu Paulo wa sita, akamteua kuwa Askofu 16 Januari 1971 na hatimaye kuwekwa wakfu 25 Aprili 1971. Baada ya kuwatumikia watu wa Mungu, Jimbo Katoliki la Njombe kwa moyo na akili zake zote, akang'atuka kutoka madarakani 8 Juni 2002.

Tangu mwanzo wa kazi yake kama askofu alijizatiti kimamilifu katika kazi ya kulilea Jimbo changa, kulitunza na kulielendeleza kwa hali na mali. Kwa miaka yote katika kazi yake aliongoza kwa busara, upole uvumilivu na unyenyekevu akishirikiana vema na wachungaji wote Wamisionari na wazalendo, watawa na walei bila ubaguzi. 

Marehemu Askofu Raymond Mwanyika atakumbukwa na wengi kutokana na mchango wake mkubwa wa maendeleo endelevu kwa wananchi wa Njombe. Amezikwa katika Kanisa la Kiaskofu jimboni Njombe.

No comments:

Post a Comment