| Maelezo ya benki juu ya fedha za kijiji cha Ihemi zinazodaiwa kukwapuliwa na mwenyekiti wa kijiji hicho. |
MWENYEKITI wa kijiji cha Ihemi
Kata ya Mgama Wilaya ya Iringa vijijini Castory Likwiluka amevuliwa madaraka
kutokana na matumizi yake mabaya ya madaraka kutumia mali za kijiji bila idhini
ya wanakijiji.
Katika mkutano uliofanyika kijijini hapo leo wanainchi walilazimika kumpumzisha mwenyekiti huyo ili kulinda mali za kijiji zisitumike vibaya kwa maslahi binafsi.
Miongoni mwa tuhuma zilizomuondoa
madarakani ni kutumia muhtasari bandia na kuchukua pesa benki kiasi cha
shililingi 840,000/= pamoja na shilingi 450,000/= za ulinzi wa nguzo za umeme
gredi ya taifa ambazo kampuni ya umeme (TANESCO) hulipa kijiji kwa ulinzi na
kufikisha jumla ya shilingi 1,290,000/= ambazo mwenyekiti huyo ametumia bila
ridhaa ya wananchi.
Akisoma tuhuma za mwenyekiti huyo
kwenye mkutano, Euzebio Nyalusi amesema mwenyekiti huyo amekuwa na kawaida ya
kuamua mambo bila kuwashirikisha wananchi na kufanya kijiji kama mali yake
binafsi.
“Mwenyekiti ameuza mashamba ya
kijiji bila kuwashirikisha wanakijiji. Licha ya kuwa mashamba yalishatolewa
hukumu na kuamriwa yarudishwe katika kijiji, mwenyekiti huyu ameyauza tena”
amesema.
Pamoja na hayo wananchi walihoji
mchango wa wawekezaji katika kijiji licha ya kuwa na wawekezaji sita ambao bila
mikataba yao kujulikana kwa wananchi.
“Hapa kijijini kuna wawekezaji
wapatao sita lakini hatujui mchango wao. Ina maana kijiji hakina mkataba nao?
Hatuoni faida ya kuwa na wawekezaji ambao hawana msaada wowote” amehoji.
Wananchi wamemlalamikia
mwenyekiti huyo anasadikiwa kuuza tofari walizofyatua kwa ajili ya kujengea shule ya
sekondari ya kata ya Mgama ambapo haijulikani idadi kamili ya tofari
zilizopelekwa shuleni hapo.
“Tunataka kujua tofari
tulizofyatua kwa ajili ya ujenzi wa shule zimekwenda wapi? Haya ni matumizi
mabaya ya nguvu za wananchi. Tunatumiwa kwa ajili ya watu binafsi na si
maendeleo ya kijiji kama inavyokusudiwa. Kwa mtindo huu hatuwezi kufika popote”
amesema na kuhoji.
Alipopewa nafasi ya kujibu tuhuma
hizo, Likwiluka alikiri kuwa na mapungufu hayo na kusema ni ubinadamu tu huku akiomba wananchi wamsamehe.
“Ni kweli kwamba hizo tuhuma
zinanihusu lakini ni ubinadamu tu. Pesa zimeshatumika na hayo mengine kwa
kweli
naomba mnisamehe” amesema.
Licha ya tuhuma hizo kuelekezwa
kwa mwenyekiti, wananchi wamedai kuwa hata ofisa mtendaji wa kijiji Aloyce
Mduda anahusika kwa kuwa naye ni miongoni kwa waliotengeneza muhtasari bandia na kuhidhinisha fedha kuchukulia benki.
Kumbukumbu zinaonesha kuwa Mduda
aliwahi kutuhumiwa kwa ubadhilifu wa fedha za kijiji cha Kiwele na kuhamishiwa
katika kijiji cha Ihemi ambako nako ameingia katika kashfa hiyo.
Wananchi wamelazimika kumteua
mwenyekiti wa muda Ezekiel Mlyuka hadi uchaguzi utakapofanyika ili kuwezesha
shughulizi zingine kufanyika.
Hata hivyo mtandao huu umefanikiwa kupata maelezo ya benki (bank statement) inayoonesha kijiji hicho
kuchukua fedha Mei 14, 2013 kwa Cheki (CHQ) No 218610 kiasi cha shilingi
840,000/= wanazozilalamikia wananchi.
No comments:
Post a Comment