WANACHAMA wa vikundi vya akiba na
mikopo wameonywa kuacha utegemezi na kuwa ombaomba kwa wanasiasa kwa madai kuwa
tabia hiyo inachangia vikundi vyao kushindwa kujiendesha na hivyo kufa mapema
baada ya misaada kusitishwa.
Mratibu wa benki za wananchi waishio
vijijini (VICOBA) Tisiana Kikoti ametoa ushauri huo ja wakati wa uzinduzi wa
kikundi cha Lugodalutali katika Kata ya
Igombavanu Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.
Kikoti alisema vikundi vingi vimekuwa
vikiwategemea wanasiasa jambo ambalo linaweza kuleta athari kubwa ambapo baadhi
ya vikundi vingine vimekufa kutokana na uongozi wa wanasiasa hao kukoma na
kuwataka wana-vicoba kujitegemea.
“Vicoba ni vyama visivyo na mlengo
wowote wa kisiasa, sasa ninawasihi msiwategemee wanasiasa au misaada kuendesha
vikundi vyenu, tunataka hivi vicoba view endelevu ili baadaye tuje tufungue
benki za Kata, lakini kama mkiegemea kwa wanasiasa mjue wanapoondoka madarakani
na vikundi vyenu vinakufa” alisema Kikoti.
Amewataka
wanavikundi kuwa wabunifu katika miradi mbalimbali ya ufugaji wa kuku, na hata
kilimo cha Uyoga, kwa kuwashirikisha wataalamu ili kupata mafunzo ya shughuli
hizo zitakazoendesha vikundi vyao.
Hata hivyo aliwatahadharisha kuwa
makini na matapeli katika kuwapokea wageni katika vyama vyao kutokana na
vikundi vingi kutapeliwa na watu waoingia kama wageni.
Baadhi vya vicoba wilayani Kilolo vimetaperiwa
kwa zaidi ya shilingi Milioni 30.
“Kuweni makini sana na mambo ya fedha,
hasa matumizi yasiyofaa muyaepuke, lakini jambo lingine ni kuhusu wageni
wanaofika hapa ninawaombeni mjihadhari sana nao kwani kuna wenzenu wa Kilolo
walipokea wageni waliojitambulisha kama ni waratibu wa vicoba, wakachangishwa
fedha shilingi Miliuoni 31 zilikwenda na maji, kwa hiyo muwaepuke sana watu
wanaifika hapa kijijini na kujiita waratibu au wanataka muchange hela” alisema.
Mkoa wa Iringa una zaidi ya shilingi
Milioni 500 zinazotokana na vicoba na vikundi 486 na wanampango wa kufungua
benki ya mkoa ya Vicona huku bodi ya ufuatiliaji wa mitaji ikiendelea na
mikakati hiyo ili kufanikisha shughuli za ufunguzi.
Naye ofisa maendeleo ya jamii Wilaya ya
Mufindi Hatibu Bwashehe alisema vikundi vingi vinashindwa kuendelea
kutokana na hali ya utegemezi, huku akiwataka wanavikundi wa VICOBA kuwa na
nidhamu ya matumizi ya fedha ili kuwa na maisha bora.
Bwashehe alisema ili kuwavutia watu
wengine waingie katika vikundi vya akiba na mikopo wanachama wake wanatakiwa
kuwa tofauti kimaendeleo na siyo kuwa na maisha yanayofanana na wale wasio
katika vikundi.
“Ndugu zanguni, mkitaka kufanikiwa
kuwavuteni hawa wasiotaka kujiunga, kwanza kuweni na nidhamu ya matumizi ya
fedha ili hela mnayokopeshana iweze kufanya mambo ya maendeleo, itakuwa ni aibu
kwenu kama hamtakuwa na maisha ya mfano na wengine watoto wenu wakifukuzwa
shule kwa kukosa ada, hawa hawataona umuhimu wa kujiunga katika vicoba yenu” alisema
Bwashehe.
Aliwataka wananchi wote kujiunga katika
vikundi hivyo ili kujiondoa katika maisha duni ya umasikini na kuwa wanachama
wanatakiwa kuwa makini katika kutafuta wafadhili makini ambao hawatawageuza
kuwa watumwa.
Kwa upande wake mratibu wa Vicoba
Wilaya ya Mufindi Scola Mitimingi alisema Wilaya ina vikundi 26 na tayari wana jumla
ya akiba ya shilingi Milioni 5.4 na kuwa lengo kuu la kuhamasisha wananchi hao
kujiunga katika vikundi ni kuondokana na maisha duni yanayotokana na kilimo cha
jembe la mkono, kwani baada ya kupata mtaji mkubwa kila mwanachama atakopeshwa
zana bora za kilimo.

No comments:
Post a Comment