![]() |
| Mbunge wa Njombe Kaskazini Deo Sanga (Japeople) akijibu maswali aliyoulizwa na mtandao huu. |
VUGUVUGU la wananchi kutaka mabadiliko ili kuleta maendeleo
linazidi kuchukua sura mpya katika maeneo mbalimbali mijini na vijijini baada
ya wananchi kuwataka viongozi wao watimize ahadi walizowaahidi wakati wa
kampeni za uchaguzi.
Wananchi wa kata ya Lupembe iliyopo Mkoa wa Njombe wamewajia juu baadhi ya viongozi
wa serikari kwa kuwataka kuwa wakweli kwa kile walichokiita kuwa ni kushindwa
kutimiza ahadi zao walizoziahidi katika kipindi cha kampeni za uchaguzi mwaka
2010.
Wakizungumza na mtandao huu kwa nyakati tofauti wakazi wa kata za
Mfiliga na Lupembe wamemkumbusha Rais Jakaya Kikwete kutimiza ahadi yake aliyoiahidi
wakati wa uchaguzi kwamba atakapo
chaguliwa kuwa rais atakuwa na uwezo wa kuishawishi mahakama kumaliza mgogoro
uliopo katika kiwanda cha chai Lupembe.
Wakati wa kampeni za uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 Rais Kikwete aliwaahidi
wananchi wa Lupembe kuwa akiwa rais atamaliza mgogoro huo wakati akiwahutubia
wananchi hao kwenye mkutano uliofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi
Wanyingi.
Rais Kikwete aliahidi kuihimiza mahakama kuharakisha kutoa majibu
ya kesi ya kiwanda hicho jambo ambalo halijafanyika hadi sasa huku chaguzi
zingine zikikaribia kuanza.
Walisema kumekuwapo na sitofahamu juu ya utekelezaji wa ahadi hiyo
na nyingine nyingi zilizotumika kuwanadi wagombea katika kipindi cha kampeni
mwaka 2010 jambo ambalo linazua hofu ya kuendelea na maisha magumu kwa wananchi
hao.
“Ni kweli kwamba tunatambua kiwanda cha chai Lupembe kesi yake ipo
mahakamani na hatutaki rais aingilie uhuru wa mahakama bali bali tunachotka atimize
ahadi yake ya kuihimiza mahakama katika kutoa haki ya kesi hiyo kama
alivyoahidi” walisema.
Pamoja na kumlalamikia rais juu ya ahadi hiyo, wamemtuhumu Mbunge wa jimbo la Njombe Kaskazini Deo Sanga
alimaarufu kama “Ja People” kuwa aliahidi kulishughulikia jambo hilo pindi
atakapochaguliwa kuwa mbunge.
Inaelezwa kwamba Mbunge huyo alitoa ahadi hiyo mara kadhaa katika
mikutano mbalimbali ya kampeni za kujinadi kwake na kwamba hadi sasa hakuna
maendeleo yoyote kuhusu ahadi zake huo.
Akijibu hoja hiyo Deo Sanga alikiri kuwa ni kweli kwamba
ahadi hiyo ilizungumza katika kampeni zake na zile za Rais na juhudi za
kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huo zinaendelea japo kuwa hakuziainisha.
“Zipo ahadi nyingi ambazo ziliahidiwa kipindi cha kampeni yangu na
rais kwa wananchi wa jimbo la Njombe Kaskazini kama walivyo kueleza wananchi, lakini
pia zipo ambazo tayari zimekwisha tekelezwa kwa kiwango kikubwa na nyingine
bado zingali zinaendelea kufanyiwa kazi’ alisema Sanga.”
Kuhusu mgogoro uliopo kati ya mwekezaji na wakulima wa kiwanda cha
chai Lupembe, alisema uamuzi wa mahakama kuhusu kesi hiyo kwa sasa ipo
ukingoni.
Kiwanda cha chai Lupembe kilifungwa miaka kadhaa iliyopita
kufuatia mgongaro wa kimasilahi uliojitokeza kati ya mwekezaji Nawab
Mullar dhidi ya wananchi ambao awali ndiyo waliokuwa wamiliki wa kinda hicho.

No comments:
Post a Comment