| Mbunge wa Iringa mjini Peter Msigwa akiwahutuba wakazi wa Manispaa ya Iringa katika mkutano wa hadhara uliofanyika jana katika maeneo ya Soko Kuu mkabala na Kituo Kikuu cha Polisi. |
MBUNGE wa Iringa mjini Peter
Msigwa (CHADEMA) amesema dhamira yake ya kupeleka hoja yake binafsi bungeni juu
ya ujangili wa tembo bado ipo pale pale pamoja na kuwa katika vikao vya bunge
lililopita hakupewa nafasi.
Mch. Msigwa aliyasema hayo katika
mkutano wa hadhara uliofanyika jana katika maeneo ya Soko Kuu mkabala na kituo
Kikuu cha Polisi katika Manispaa ya Iringa.
Alisema pembe za ndovu
zinazokamatwa katika kila kona ya dunia zinatoka Tanzania jambo linalotishia usalama
wa wanyama katika mbuza za Taifa.
Kutokana na ujangili huo Msigwa
ambaye pia ni Waziri kivuli wa maliasili amemtaja Katibu Mkuu wa CCM Taifa
Abdalah Kinana kuwa ni miongoni mwa watuhumiwa wa pembe za ndovu nchini.
“Wahusika wakubwa ni baadhi ya
polisi na usalama wa taifa wasiowaadilifu ambao wanajihusisha na wizi wa pembe
za ndovu” alisema.
Alisema viongozi wengi wa ngazi
ya juu katika chama cha Mapinduzi ambao leo wanajinadi kwa wananchi kuonekana
wasafi ni miongoni mwa majandili na wizia wa pembe za ndovu.
“Leo hii mtu unajiita Mnec wakati
kipindi cha baba wa Taifa alikuwa ni mtuhumiwa wa pembe za ndovu! Pia
nawashangaa watu wa usalama wa taifa, mnang’ang’ania kunasa sauti yangu katika
mikutano wakati Twiga na tembo huko wanauawa. Ni usalama gani huu?” alisema na kuhoji Msigwa.
Hata hivyo alisema zinapojitokeza
hoja za msingi ambazo ni manufaa kwa umma na kufunikwa ni wazi kuwa wapo baadhi
ya watu ambao wamezoea uongo badala ya ukweli na kwamba kilichotokea katika
vikao vya bunge lililopita ni ukiukwaji wa makusudi wa taratibu za nchi.
“Leo hii vyombo vinavyotakiwa
kulinda maadili, ndivyo hivyo hivyo vinavyotumika kuhujumu nchi. Kama mlivyoona
hoja zenu wananchi zikizimwa kule bungeni, tulichokifanya ni mwanzo ila kama hali hii itaendelea, kipo kinachokuja ambacho ni
kikubwa kuliko kile. Tunapotetea huduma za jamii wanatuambia tunafanya fujo. Ni
wenda wazimu gani huo?” alisema.
Katika hatua nyingine Msigwa
alisema vurugu na mauaji mbalimbali yanayotokea nchini kuhusishwa na imani za
kidini ni mpango wa kisiasa ambao wanasiasa wa chama cha Mapinduzi wanautumia
ili kuwagonganisha wanchi kidini.
“Kila wakati tunasikia mauaji na
vurugu za kidini, mtakumbuka juzi kuna mchungaji amechinjwa kule Geita na leo
Padri wa Kanisa Katoliki amepigwa risasi huko Zanzibar . Huu ni mpango wa CCM kutugonganisha
kidini kwa kuwa kila wanachokifanya kinagonga mwamba. Miaka 50 tumeishi kwa
kuheshimiana bila vurugu za kijinga kama hizi
lakini iweje leo katika utawala wa Kikwete uibuke udini? Huo ndio mpango wake na
yeye akiwa mhamasishaji mkubwa wa udini ili kutugonganisha” alisema.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya
Mivinjeni Frank Nyalusi (CHADEMA) alisema matatizo mengi yanayojitokeza nchini
yanasababishwa na udhaifu wa serikali iliyochoka.
“Watu wavamia maeneo kwa sababu
ya mipango mibovu ya serikali iliyopo madarakani, kuenda kwenye huduma za afya
hakuna dawa, basi wabinafsishe hospitali hizo ili tujue moja!, vituo vya polisi
vinaendesha doria kwa kuomba fedha kwa watu binafsi ili wanunue mafuta.
Wakiwaomba ninyi wananchi kama mnazo wapeni
kwa sababu serikali imeshindwa kuwahudumia” alisema Nyalusi.
Naye Mhadhiri wa chuo Kikuu cha
Arusha Dadi Igogo alisema kutokana na kauli za CCM kutaka kukomboa majimbo,
wananchi wanatakiwa kuwa makini na kauli hizo kwa kuwa hazina mantiki yoyote
katika maisha.
“Kwa miaka 50 tulikuwa na maadui
watatu ambao tulikuwa tukiwapiga vita ambao ni ujinga, Umasikini na Maradhi
lakini sasa hivi ameongezeka adui mwingine ambaye ni mbaya sana anaitwa CCM. Ndugu zangu kuweni makini
na adui huyo atatumaliza” alisema Igogo.
Alisema moja ya kauli ambazo
zinaonesha dhahiri kuwa CCM ni chama cha watu wasio na nidhamu, ni kauli za
Nape Nnauye ambazo daima yeye ni matusi hata kuwatukana wazazi wake.
“Naomba kumuuliza Nape, ina maana
upevu wake wa nidhamu umeanzia kwa Dkt. Slaa? Kama
hawezi kumheshimu Dkt. Slaa, kwani nini hajamwambia baba yake kuwa ni mtoto
wake? Sasa CCM wanapojiandaa kukomboa jimbo, Msigwa anaendelea kuwakomboa watu
wa Iringa. Wamsiwasikilize waliofilisika kufikiri na kuwajibika watawatupa motoni”
alisema.
No comments:
Post a Comment