MTUHUMIWA wa mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa habari wa kituo cha
runinga cha Channel Ten Daud Mwangosi aliyetakiwa kufikishwa mahakamani leo hakufikishwa kutokana na sababu iliyoelezwa kuwa gari la kubebea
mahabusu halikuwa na mafuta.
Akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa
Wilaya Dyness Lyimo amesema Pasificus Cleophace Simon (23) mtuhumiwa wa
mauaji ya mwandishi huyo pamoja na watuhumiwa wengine waliopo mahabusu
hawakufikishwa mahakamani kwa sababu ya gari linalotumika kuwapeleka
mahakamani hapo halikuwa na mafuta.
"Tatizo kubwa lilopo sasa hivi ni uhaba wa mafuta kwa sababu hata mimi
mwenyewe gari langu halina mafuta; sisi mafuta tunategemea mafuta kutoka
boharini na kwa bahati mbaya bohari haina mafuta" amesema.
Hata hivyo
Lyimo amesema kuwa kulikuwa na uwezekano wa kumpeleka mtuhumiwa huyo wa
mauaji ya mwandishi kwa kumsindikiza kwa miguu kutokana na gereza kuwa
jirani na mahakama lakini hawakufanya hivyo ili kuzuia kuteka hisia za
watu ambazo zingeweza kusababisha fujo.
"Kulikuwa na uwezekano mkubwa wa watuhumiwa kuletwa mahakamani kwa
miguu lakini haikuwezekana kwa sababu askari wasingeza kumchukua
mtuhumiwa mmoja na kuwaacha wengine ambao walipaswas kusomewa mashtaka
yao hapo jana" amesema.
Hata hivyo mtuhumiwa huyo mwenye namba G 2573 kila anapofikishwa
mahakamani, hufikishwa kwa gari la peke yake ambapo kwa awamu iliyopita
alifikishwa kwa gari la polisi lenye namba PT 1467 likiwa na ulinzi
mkali.
Siku ya kwanza mtuhumiwa huyo alifikishwa mahakamani hapo kwa gari la
kifahari lenye namba za kiraia T 320 ARC linalosadikiwa kuwa ni la RCO
huku kwa mara ya pili akifikishwa kwa miguu na kuondolewa mahakamani
hapo kwa gari namba DFP 2175 pick up akiwa katika ulinzi mkali.
Kwa mujibu wa hakimu huyo, kesi imeahirishwa hadi Novemba 21 mwaka huu itakapotajwa tena.
No comments:
Post a Comment